Wednesday, February 12, 2014

KIUNGO wa zamani wa kimataifa wa Tanzania, Sekilojo Johnson Chambua amesema kwamba Yanga SC inaweza kuitoa Al Ahly katika Raundi ya Kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika, kwa kuwa soka ya Misri hivi sasa imeshuka tofauti na miaka ya nyuma enzi zao wanacheza, lakini wanatakiwa kufanyia kazi mambo matatu.Akizungumza na BIN ZUBEIRY leo mchana, Chambua amesema kwamba Yanga ina matatizo matatu, kwanza hawamudu kucheza dakika 90 kwa kasi ile ile, pili safu ya ulinzi inakatika na safu ya ushambuliaji haina makali ya kutosha, mambo ambayo kama watayafanyia masahihisho, wanaweza kuweka historia kwa kuwa timu ya kwanza ya Tanzania kuitoa mashindanoni Ahly.Magwiji; Sekilojo Chambua kulia akiwa na Edibily Lunyamila enzi zao miaka ya 1990“Mara ya mwisho nimeiona Yanga inacheza na Mbeya City pale Uwanja wa Taifa, wakashinda bao 1-0. Niseme tu Yanga ilicheza vizuri, lakini washambuliaji wake walikosa mabao mengi kutokana na kukosa ubunifu wanapofika kwenye eneo la wapinzani,”alisema kiungo huyo wa zamani wa Tukuyu Stars ya Mbeya na Yanga SC ya Dar es Salaam.Chambua alisema mchezaji David Luhende anayetumika kama winga wa kushoto kwa sasa pamoja na Simon Msuva anayecheza kulia, walikuwa wanapata mipira ya kuingia nayo kwenye boksi, lakini wakawa ama wanatia krosi au wanarudi nyuma. “Hawakutakiwa kufanya vile, walitakiwa kufanya kama ambavyo Edi (Edibily Lunyamila) alikuwa anafanya wakati ule tunacheza naye, alikuwa anaingia ndani. Kitendo cha kupiga krosi tu kinawapa nafasi hata mabeki kuokoa, lakini kama wangekuwa wanaingia ndani wangeweza kufunga au kutengeneza nafasi za wengine kufunga,”.  Chambua alisema kwamba iwapo mawinga hao wa Yanga watabadilika na kuingia na mpira kwenye eneo la hatari la wapinzani, kasi ya mashambulizi ya Yanga itaongezeka na hiyo inaweza kuzalisha mabao mengi.Lakini Chambua alimpongeza mshambuliaji Mrisho Khalfan Ngassa anavyocheza hivi sasa, kwamba anakosa tu mtu wa kushirikiana naye pale mbele, ila makocha wa Yanga kama watampatia ‘pacha’ mzuri mchezaji huyo, safu ya ushambuliaji ya timu hiyo itakuwa hatari zaidi.Kuhusu safu ya ulinzi, Chambua alisema kwamba mtu mmoja tu anacheza vizuri kwa sasa, ambaye ni beki wa kushoto, Oscar Joshua lakini wengine haswa mabeki wa kati wanatakiwa sana kurekebisha uchezaji wao.“Mabeki wa kati wa Yanga wanakatika sana, sasa ile ni hatari mno unapokutana na timu kama Ahly yenye uwezo mkubwa wa fikra, mbinu na ufundi. Kwa kweli, Yanga lazima wabadilishe staili ya uchezaji wao kama kweli wanataka kuitoa Ahly, hili  ni jambo ambalo makocha wanatakiwa kulifanyia kazi mapema sana,”alisema.Chambua pia aliisifu Mbeya City na kusema kwamba hiyo Tukuyu Stars mpya mkoani humo, lakini akawashauri waboreshe mbinu za kiufundi.“Siku wanacheza na Yanga, wachezaji wa Yanga walikuwa wanafanya makosa mengi sana ambayo kama Mbeya City ingekuwa vizuri sana kiufundi, ingeyatumia kusawazisha na hata kuongeza bao,”alisema.Yanga SC inaweza kukutana na Al Ahly mwezi ujao katika Raundi ya Awali ya Ligi ya Mabingwa Afrika, iwapo itamalizia vyema Raundi ya Awali mwishoni mwa wiki hii, baada ya Jumamosi kuitandika mabao 7-0 Komorozine ya Comoro katika mchezo wa kwanza wa Raundi ya Awali Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.


Posted via Blogaway

0 comments:

Post a Comment